KWANINI SHERIA HAIWABANI WANAOKAA VITI VYA NYUMA KUFUNGA MKANDA?

Na Adrian mgaya
Shirika la afya duniani linataja viashiria vikuu vya ajali za barabarani kuwa ni kutokuvaa kofia ngumu kwa waendesha pikipiki, mwendokasi usiofaa, matumizi ya vilevi kwa madereva, kutotumia vizuizi vya watoto na kutofunga mkanda wa usalama katika vyombo vya usafiri.
Pamoja na viashiria hivi kutajwa kuwa ni vyanzo vikuu vya ajali na kuongezeka kwa madhara ya ajali za barabarani bado sheria mama ya usalama barabarani nchini Tanzania, haijagusia kiundani mambo haya ili kuendana na matakwa ya umoja wa mataifa kupitia shirika la afya duniani.
Ambapo wanapendekeza sheria madhubuti zitasaidia kupunguza vifo na majeruhi wa ajali katika barabara zetu.
Edda sanga, Mkurugenzi mtendaji wa TAMWA anasema "Umoja wa mataifa na shirika la afya duniani wanakiri kwamba sheria madhubuti zinahitajika katika kupunguza idadi ya watu wanaofariki katika barabara zetu. Tanzania lazima tuwe na sheria kali za usalama barabarani kukomesha hali hii”
Sheria ya usalama barabarani ya mwaka 1973 ambayo ilifanyiwa marekebisho mwaka 2002 nchini Tanzania, ina mapungufu ambayo kwa namna moja ama nyingine hukwamisha mpango wa kutokomeza ajali za barabarani pamoja na madhara yake.
Kwa mfano sheria ya usalama barabarani ya mwaka 1973 ambayo ilifanyiwa marekebisho mwaka 2002 imewasahau kabisa abiria wanaokaa viti vya nyuma, katika kifungu cha 39(11) kinatoa mwanya kwa abiria wa viti vya nyuma kutofunga mkanda.
Kwa mujibu wa kifungu hiki dereva na abiria wa mbele ndio wanaotakiwa kufunga mkanda huku wale waliokaa nyuma wakiachwa huru.
Ripoti  ya mwaka 2015 ya shirika la afya duniani katika masuala ya usalama barabarani inaeleza kuwa  ufungaji sahihi wa mkanda hupunguza madhara pindi ajali inapotokea zaidi ya ASILIMIA  50% kwa dereva na abiria wa viti vya mbele na zaidi ya 75% kwa abiria wa viti vya nyuma.
Mary Kessi, mratibu wa mradi maalumu wa usalama barabarani nchini Tanzania kutoka shirika la afya duniani, ofisi za Dar es salaam, ambapo kwa sasa wanashughulika na mabadiliko ya sheria za usalama barabarani, anasema...
"Unapokuwa umefunga mkanda unakuwa salama zaidi pindi ajali itakapotokea tofauti na usipofunga”…
Anaendelea kueleza kuwa "tumeshirikiana na wadau mbalimbali tumeweza kufanya utafiti na kubaini kuna mapungufu katika sheria zetu, hivyo tunaishauri serikali kufanya marekebisho katika sheria ili kuondoa baadhi ya mapungufu", anasema.
Utafiti huu unaungwa mkono na takwimu za ajali za barabarani zinazotolewa na jeshi la polisi kikosi cha usalama barabarani.
Ambapo mwanasheria wa jeshi la polisi kikosi cha usalama barabarani ASP Deus Sokoni  anaweka wazi kuwa madhara huwa ni makubwa zaidi pindi ajali zinapotokea wale wasiofunga mkanda hupata madhara makubwa ukilinganisha na wale waliofunga mkanda.
Tarehe 28 ya mwezi Mei 2017 ni siku ambayo imeacha historia  kwa Jasmin Mdoe shabiki wa timu ya Simba ambaye alikuwa katika gari ndogo binafsi lililopata ajali maeneo ya Dumila, Morogoro wakitokea Dodoma.
Jasmine anaeleza kuwa wakiwa wanatoka kuangalia mchezo wa soka kati ya Simba na Mbao wakiwa na furaha tele baada ya timu yao (Simba) kuibuka na ushindi katika mchezo huo uliochezwa mjini Dodoma, furaha yao iligeuka majonzi ghafla.
Gari walilopanda lilipasuka gurudumu la mbele na kupinduka. Jasmine anaeleza kuwa ajali ile ilikatisha Maisha ya rafiki yake aliyejulikana kwa jina la Shose Fidelis, na rafiki zake wengine wakiachwa na majeruha.
“Shose, alikaa kiti cha nyuma kabisa na hakufunga mkanda. Sisi wengine tulifunga mikanda, licha ya gari kupinduka mara tatu ila tulibaki katika viti vyetu,” anasimulia Jasmine Mdoe.
Licha ya hatari inayoweza kutokea, baadhi ya abiria wanaotumia magari binafsi hawafungi mikanda ya usalama hasa wanaokaa katika viti vya nyuma kutokana na sababu mbalimbali,
Lakini huenda sheria ingekuwa na sehemu inayolazimisha kufunga mkanda kwa abiria wote jambo hili jambo hili lisingekuwepo.
Ras Lumelezi mkazi wa Bagamoyo anasema“mimi naona kuna umuhimu wa kufunga mkanda kwa sababu huwezi kujua dereva anaeendesha hilo gari amelewa, au hilo gari linaweza kuwa na hitilafu ya kiufundi”
Vilevile anaeleza “ajali inaweza ikatokea muda wowote, lakini kuna vitu ambavyo tunaweza kuchukua kama tahadhari ikiwemo kufunga mikanda, hata kama ajali itatokea basi madhara yasiwe makubwa…”
Kwa upande wake Musa Jumanne mwanafunzi wa darasa la tano katika shule ya msingi Assumption mkoani Arusha anasema kuwa kila siku asubuhi anatumia usafiri wa daladala kwenda shule lakini siku zote huwa anapata kigugumizi  “Dereva na abiria wa mbele wanafunga mkanda nashangaa kwanini wasiweke mikanda na viti vya nyuma?” anauliza Musa Jumanne.
Kwa mujibu wa ripoti ya usalama barabarani yam waka 2015 iliyotolewa na umoja wa mataifa kupitia shirika la afya duniani Tanzania ni miongoni mwa nchi za ukanda wa afrika mashariki zilizo na sheria ambayo haigusi abiria wote katika suala la ufungaji mkanda wa usalama.
Nchi za Kenya na Uganda zinatajwa kuwa na  sheria madhubuti inayowataka abiria wote wawe wamefunga mkanda ambayo huenda inabana watumiaji wa magari kutofunga mikanda ya usalama. Swali ni lililo vichwani mwa wengi ni lini Tanzania itakuwa na sheria imara katika ufungaji wa mikanda.
Mwanahabari mkongwe ambaye kwa sasa anafanya kazi Televisheni ya Taifa TBC 1, Tuma Provian Dandi yeye ni muathirika wa ajali za barabarani, anasema “pamoja na kuwa kuna sheria za usalama barabarani, lakini nina imani zingine zimechakaa” …
Anaendelea kusema… “mathalani sheria ya kufunga mkanda inamuamuru dereva na abiria wa mbele wawe wamefunga mkanda, nadhani imefika wakati sasa hii sheria ifanyiwe marekebisho yaani iwe kosa kwa abiria yoyote kukaa kupanda gari bila kufunga mkanda”
Ukimya sheria ya usalama barabarani juu ya umuhimu na ulazima wa kufunga mkanda wa usalama kwa abiria wa viti vya nyuma si tu unawanyima abiria haki ya kujilinda bali unaongeza idadi ya utegemezi kwa waathirika wa ajali za barabarani,
Na ndio maana asasi mbalimbali za kiraia kama vile TAMWA, TAWLA, SHIVYAWATA, Road safety ambassadors(RSA), AMEND na Tanzania Lawyers Society (TLS) zimekuwa zikipigia kelele mabadiliko ya sheria.
Mabhezyo Rehani mwanasheria kutoka Tanzania Lawyers Society(TLS) anaeleza kwamba “Sheria yetu ipo kimya juu ya ufungaji mkanda kwa abiria wa nyuma,”
“na unaweza ukaona sheria mama inakinzana na sheria nyingine ambazo zimeshakuja mbele ya sheria mama ambazo zinagusia abiria wote wale wa mbele na wa nyuma, kwa hiyo ni vizuri pia sheria mama ikaaweka ulazima wa abiria wote kufunga mkanda”.
Kauli hii inaungwa mkono na mwenyekiti wa mabalozi wa usalama barabarani nchini John Seka ambaye anaona mabadiliko ya sheria, yanaweza kupunguza madhara yanayotokana na ajali za barabarani kutokana na kutofunga mkanda.
Mchakato wa mabadiliko ya sheria ya usalama barabarani haukwepeki, mwenyekiti wa kamati maalumu ya kurekebisha sheria ya usalama barabarani, ambaye pia ni wakili na mwanasheria wa jeshi la polisi ASP Deus Sokoni, anaeleza kuwa hatua zote katika mchakato wa kubadilisha sheria za usalama barabarani zikikamilika zitapelekwa bungeni Bungeni ili kuridhia iwe sheria.
Hata hivyo mbali na sheria ya usalama barabarani kuwa na mapungufu bado watumiaji wanatakiwa kuangalia zaidi usalama wao kwa kuzingatia kufunga mkanda, kwani wahenga walisema kinga ni bora kuliko tiba

Makala hii imeandikwa na Adrian Mgaya mhitimu wa chou kikuu cha Dar es salaam, katika shahada ya uandishi wa habari (B.A in Journalism) ambaye ni mnufaika wa mafunzo ya uandishi wa habari za usalama barabarani katika mradi wa WHO bloomberg initiative for global road safety,yanayoendeshwa na Tanzania Media Foundation (TMF) anapatikana kwa 0656110670 au mgayaadrian@gmail.com



Comments

Popular posts from this blog